Friday, January 29, 2010

Mwanza waipania Simba

Na Jacqueline Massano

KAMANDA wa Polisi wa mkoa wa Mwanza, Jamal Rwambow amesema iwe isiwe ni lazima timu ya Toto African iifunge Simba ili kujinusuru isishuke daraja kutokana na kuwa na pointi chache kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara inayoendelea kwenye vituo mbalimbali.
Simba inayoongoza kwenye msimamo wa Ligi kwa kuwa na pointi 39 inatarajia kushuka dimbani kesho kumenyana na Toto kwenye mechi inayotarajia kufanyika kwenye uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza.
Kamanda Rwambow alisema kutokana na jitihada walizozifanya za wananchi kuichangishia timu hiyo ili isishuke daraja ana imani inaweza kuifunga Simba siku hiyo ya Jumapili.
"Simba haiwezi kutoka Mwanza, iwe isiwe ni lazima ifungwe tu. Haiwezekani ije Mwanza halafu iondoke na ushindi huku kwetu," alisema Kamanda huyo ambaye pia ni shabiki mkubwa wa Simba.
Rwambow alisema kama timu hiyo iliweza kuifunga Simba msimu uliopita ilipoenda kucheza Mwanza, na sasa hivi wanataka kuendelea kuifunga tena. "Mzunguko wa kwanza ilitufunga kwa sababu ilikuwa Dar lakini nawaambia hivi tutawafunga tena. Ni kweli mimi naipenda Simba lakini ni lazima tuifunge," alisema
Alisema juhudi zote hizo ni kuinusuru timu hiyo ili iweze kucheza ligi kuu na kuwafanya wakazi wa Mwanza waweze kuziona timu za Simba na Yanga zikienda Mwanza kucheza soka na wala si vinginevyo.
"Tukifanya mchezo wakazi wa Mwanza watakuwa hawazioni tena timu za Simba na Yanga, na ndiyo maana na wenyewe waliamua kuichangia na kuisaidia Toto pale ilipokwama na hii yote ni kuitaka timu yao ibaki kwenye ligi," alisema
Alisema kwa sasa timu yao ina pointi nane kwenye msimamo wa ligi, kutokana na hali hiyo watafanya juhudi ili iliweze kushinda mechi zake zote saba ambazo anachezea nyumbani. "Tuna mechi saba nyumbani, hizi ni lazima tushinde, na tukishinda zote tutakuwa na pointi 28 hivyo itakuwa si rahisi kushuka daraja tena," alisema
Kamanda huyo alisema ikiwa itashindikana na timu ikashuka daraja watakuwa hawana jinsi itabidi waombe radhi kwa wakazi wa Mwanza na kujipanga upya ili timu iweze kupanda daraja tena.

Sunday, January 3, 2010

Stars vs Ivory Coast leo

#Wadau waitabiria makubwa Stars

WADAU mbalimbali wa soka nchini, wameitabiria timu yao ya taifa, Taifa Stars itajifunza mambo mengi ya kisoka pale itakapocheza mechi ya kimataifa ya kirafiki dhidi ya 'Tembo' wa Ivory Coast. Mechi hiyo inayosubiriwa kwa hamu kubwa na wapenzi wa soka nchini, itafanyika katika uwanja wa Taifa saa 1.30 usiku.
Mshauri wa timu ya soka ya Villa Squad ya Dar, Kenneth Mwaisabula, alisema mechi hiyo ni fursa nzuri kwa wachezaji wa Stars kujifunza mambo mengi kutoka kwa wapinzani wao.
"Ivory Coast ina wachezaji wengi wa kulipwa, wanafahamu mbinu mbalimbali za soka, hivyo vijana wetu wanatakiwa kuwa makini na kuangalia makosa yao ili waweze kujifunza toka kwa wenzao," alisema Mwaisabula.
Alisema mechi dhidi ya timu kubwa zenye wachezaji wa kulipwa, ni nzuri kwa timu zetu kwa kuchukua mbinu na mafunzo toka kwao na kuepukana na soka la kizamani.
mdau mwingine wa soka, Nassor Duduma katibu msaidizi wa zamani wa Yanga, alisema mechi ya leo ina malengo tofauti kwa wachezaji wa timu zote mbili huku Ivory Coast ikiwa katika maandalizi ya fainali za mataifa ya Afrika huko Angola na Stars kujifunza.
"Stars lengo lake katika mechi hiyo ni kuonyesha wanaweza na kujifunza kwa kupambana na Drogba (Didier) na Toure (Kolo), lakini wageni wanaangalia zaidi katika fainali za kule Angola," alisema Duduma.
Wakati Duduma akisema hayo, mdau mwingine wa Jijini Mwanza, Jamal Rwambow, alisema mchezo wa leo ni muhimu kwa Stars kwa sababu utatoa nafasi ya wachezaji wetu kujifunza mengi.
"Siwapi nafasi Ivory Coast ya kutushinda, lakini naamini tunaweza kutoka sare ama kushinda mechi hiyo," alisema Rwambow ambaye ni Kamanda wa Polisi mkoani Mwanza.
Aidha, alisema wachezaji wa Stars wanatakiwa kujiamini na kucheza bila woga na kuweza kuepuka majina ya wachezaji wakubwa wanaocheza soka Ulaya.
Hata hivyo, kocha maarufu nchini, Syllersaid Mziray, alipotakiwa kuzungumzia mechi hiyo, alisema kwa ufupi "Sina la kuzungumza".
Mziray ambaye amekuwa akiipinga mechi hiyo kwa madai Stars haitajifunza lolote, safari hii ameonekana kuwa mkimya zaidi.